Pages

Friday, September 18, 2015

UTT YAPOKEA TUZO YA UTENDAJI NA USIMAMIZI BORA


Watanzania wametakiwa kujitokeza kwa wingi na kuwekeza katika Mfuko wa Umoja ili kuongeza faida zitakazoleta tija katika kukuza uchumi wa taifa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko huo, Dk Hamis Kibola alitoa wito huo jana wakati akizungumzia mafanikio yaliyopatikana ndani ya mfuko huo kwa muda wa miaka kumi tangu kuanzishwa kwake.Dk Kibola alisema kwa miaka kumi Mfuko huo umeweza kutoa faida kwa wawekezaji huku kukiwa na ongezeko la rasilimali zilizopo kwenye mfuko huo kutoka Sh90.5 bilioni mwaka 2005 hadi Sh217 bilioni Septemba mwaka huu. 

“Watanzania wamekua na wasiwasi wa kuwekeza kwa kuhofia kushuka na kupanda kwa vipande, lakini kwa miaka kumi mfuko wetu haujawahi kuhatarisha pesa za muwekezaji”, alisema Dk. Kibola na kuongeza,“Watanzania walete pesa zao ili wapate kufaidika na mfuko wetu, kwa miaka kumi wawekezaji wa kawaida wamenufaika kwa kupata marejesho mazuri kwa kuwa mfuko wetu umekua wa mafanikio makubwa. Hii itawasaidia watanzania kuwa na tabia ya kuweka akiba mara nyingi wawezavyo”.

Katika mkutano huo, Bodi ya UTT/AMIS ilipokea tuzo ya Utendaji Bora na Usimamizi wa Mifuko ambayo ilitolewa na taasisi ya Capital Finance International (CFI). Mkurugenzi mtendaji wa CFI, Anthony Michael alisema tuzo hiyo hutolewa kwa mashirika na makampuni ambayo yamekua yakifanya vizuri na Bodi hiyo imefanya vizuri katika utekelezaji na usimamizi wa mifuko yao mitano.

“Taasisi yetu inafanya tafiti katika mashirika na makampuni mbalimbali ambayo yanafanya kazi vizuri. Tanzania ni moja kati ya nchi zinazovutia, na kwa miaka kumi bodi ya UTT/AMIS imefanya kazi yenye mafanikio kwa bidii sana”, alisema Michael.

Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Profesa Joseph Kuzilwa alisema zawadi hiyo itaongeza chachu katika utendaji wa kazi zao huku akiongeza kuwa wamejipanga kuwafikia watanzania wengi zaidi.

No comments:

Post a Comment